Katika ujumbe alioweka kwenye mtandao wa X, Netanyahu ameukosoa Umoja wa Mataifa kwa kuliweka jeshi la Israel kwenye orodha yake nyeusi, akisema "UN imejiweka kwenye orodha nyeusi ya historia ilipokubali madai ya kipuuzi ya Hamas." Licha ya vita vya kikatili na kinyama vilivyoanzishwa na jeshi la utawala wa Kizayuni wa Israel tangu Oktoba 7 mwaka jana vilivyoandamana na mauaji ya kimbari ya Wapalestina wasio na ulinzi wa Ukanda wa Ghaza, Netanyahu amedai katika andiko lake hilo kuwa eti jeshi la Israel "ndilo jeshi lenye maadili zaidi duniani" na akaongezea kwa kusema: "hakuna uamuzi wa ardhi tambarare wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa unaoweza kulibadilisha hilo." Utawala wa Kizayuni wa Israel umeendeleza mashambulizi yake ya kikatili dhidi ya Ghaza licha ya azimio la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kutaka kusitishwa mapigano mara moja katika eneo hilo la Palestina lililowekeza mzingiro.
Zaidi ya Wapalestina 36,700 wameuawa shahidi hadi sasa huko Ghaza, wengi wao wakiwa wanawake na watoto, na wengine zaidi ya 83,500 wamejeruhiwa.
Miezi minane ikiwa imepita tangu utawala wa Kizayuni ulipoanzisha vita vya kikatili dhidi ya Ghaza, sehemu kubwa ya majengo ya eneo hilo yamegeuka magofu huku jeshi la Kizayuni likiendelea kuweka kizuizi cha kufikishwa chakula, maji safi na dawa kwa wakazi wa eneo hilo wanaoatilika kwa njaa. Utawala wa Kizayuni umeshtakiwa na unashutumiwa kwa mauaji ya kimbari katika Mahakama ya Kimataifa ya Haki ICJ, ambayo uamuzi wake wa hivi karibuni umeiamuru Tel Aviv isitishe mara moja operesheni yake ya kijeshi katika mji wa kusini wa Rafah, ambako zaidi ya Wapalestina milioni moja walikimbilia kutafuta hifadhi kutokana na vita kabla ya mji huo nao kuvamiwa Mei 6.../
342/